Stori: mwadishi wetu SIRI
nzito imevuja! Ni dhahiri kwamba, Rais Jakaya Kikwete ‘JK’ hatavunja
baraza la mawaziri kufuatia kusitisha kwake uteuzi wa mawaziri wanne na
kifo cha aliyekuwa Waziri wa Fedha, Mipango na Uchumi, Dk. William
Augustao Mgimwa kama wengi wanavyoamini bali atabadilisha tu, Risasi
Jumamosi lina cha kushika mkononi.
Rais Jakaya Kikwete ‘JK’.
Mawaziri ambao uteuzi wao ulitenguliwa ni
Emmanuel John Nchimbi (Mambo ya Ndani), Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na
Jeshi la Kujenga Taifa), Mathayo David Mathayo (Maendeleo ya Mifugo na
Uvuvi) na Balozi Khamis Juma Kagasheki (Maliasili na Utalii)
aliyejiuzulu kutokana na ukiukwaji wa maadili na haki za binadamu katika
Oparesheni Tokomeza Ujangili.
Waziri Mkuu, Mh. Mizengo Pinda.
KWA NINI HAVUNJI BARAZA?
Kwa mujibu wa chanzo cha ndani serikalini, JK hana mpango huo kwa
sababu kuu mbili. Kwanza kuvunja baraza la mawaziri ni kumuweka kando
waziri mkuu wa sasa, Mizengo Kayanza Peter Pinda na kuteua waziri mkuu
mwingine.
Pili, atakuwa anaongeza mzigo kwa serikali kwa kuwa
waziri mkuu akiondoka madarakani huendelea kulindwa na serikali na
kupokea stahiki zake mbalimbali.
Mhe.Nchimbi.
NI NYERERE Tangu Muungano wa Tanganyika na
Zanzibar, ni Baba wa Taifa tu, hayati Mwalimu Julius Nyerere ndiye
aliyewahi kuwa na mawaziri wakuu wanne.
Alianza na Rashid Mfaume
Kawawa, akafuata Edward Moringe Sokoine, Salim Ahmed Salim (baada ya
kifo cha Sokoine) na Cleopa David Msuya.
Shukuru Kawambwa. AWAMU YA MWINYI Katika awamu ya pili, Rais Ally Hassan Mwinyi, mawaziri wakuu walikuwa Joseph Warioba, John Malecela na David Msuya.
Katika awamu ya tatu ya Rais Benjamin William Mkapa kulikuwa na waziri wakuu mmoja tu, Frederick Tuluwayi Sumaye.
WAZIRI MKUU HADI 2015
Kwa sababu hiyo, chanzo kikasema kuwa Pinda ataendelea ‘kuula’ kwenye
nafasi yake ya kuwa waziri mkuu wa Tanzania hadi mwisho wa muhula wa
awamu ya nne, mwaka 2015.
WATAENDELEA KUPANGUA
Hata hivyo, kwa mujibu wa chanzo hicho, JK na rais ajaye wataendelea
kukumbwa na shinikizo la kupangua baraza la mawaziri kila wakati
kutokana na mfumo wa madaraka uliopo sasa.
“Unajua mfumo wa sasa uko
hivi; waziri anateuliwa na rais, katibu mkuu wa wizara pia anateuliwa
na rais. Katibu mkuu wa wizara ana uwezo wa kumfukuza kazi mkurugenzi wa
halmashauri bila waziri kujua, lakini waziri hana uwezo huo.
“Nguvu
kubwa ya kazi ipo kwa makatibu wakuu ambao ndiyo watendaji wakubwa wa
wizara. Kinachotokea ni kwamba kama wizara itampata waziri mwenye
kusimamia sawa majukumu yake kiasi cha kutishia ulaji wa makatibu wakuu,
atawekewa zengwe mpaka ang’oke.
“Ndiyo maana utakuta mawaziri
kwenye wizara kila siku wanawajibika kisiasa lakini makatibu wakuu wapo
tu. Ni mfumo mbaya wa kimadaraka hivyo JK atabadili kila siku, hata rais
ajaye naye atakuwa katika harakati hizo,” kilisema chanzo hicho.
MAWAZIRI ZAIDI
Chanzo kikaenda mbele zaidi kwa kunyetisha kwamba, wapo mawaziri ambao
wanakalia kuti kavu na huenda wakang’olewa kabisa kutokana na utendaji
kazi wao usioridhisha.
SHUKURU KAWAMBWA Huyu anadaiwa kung’oka wakati wowote kutokana na madai ya walimu.
Chanzo kilisema kuwa Kawambwa pia anaponzwa na mfumo kwani kwa kawaida
mwalimu anaajiriwa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi lakini
usimamizi wake unakuwa chini ya Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa (Tamisemi).
Ikadaiwa kuwa mwalimu anapandishwa cheo na Wizara
ya Utumishi, lakini mshahara analipwa na Wizara ya Fedha, Mipango na
Uchumi (hazina).
“Sasa mwalimu akipandishwa cheo na utumishi,
nyongeza ya mshahara inatakiwa itoke hazina. Hazina nao wanakuwa hawana
habari kwa sababu ya mawasiliano duni, matokeo yake mwalimu analia na
mwajiri wake ambaye ni Wizara ya Elimu. Hili la walimu litamng’oa
Kawamba,” kilisema chanzo.
Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, mama Anne Kajumulo Tibaijuka.
ANNA TIBAIJUKA Chanzo kilidai kwamba Waziri wa
Ardhi na Maendeleo ya Makazi, mama Anne Kajumulo Tibaijuka naye yupo
mguu pande, sawa kwa sababu ya migogoro ya wakulima na wafugaji.
Mfano: “Wakulima wanaopakana na Kiwanda cha Mbolea cha Minjingu,
Manyara, wamekuwa wakilalamikia kitendo cha mazao yao kuunguzwa na
mbolea hiyo, waziri ameshaambiwa akajibu atafuatilia, sasa atafuatilia
mpaka lini?
“Kuna kamati iliundwa kufuatilia suala hili. Pia
inadaiwa kuwa vigogo mbalimbali wa serikali wamejimegea maeneo makubwa
ya ardhi mkoani Morogoro hivyo kusababisha migogoro isiyoisha kati ya
wakulima na wafugaji wanaogombea ardhi kiduchu iliyobaki, huenda ikawa
miongoni mwa mambo yatakayomng’oa madarakani Mheshimiwa Tibaijuka,”
kilisema chanzo.
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza.
CHRISTOPHER CHIZA Huyu ni Waziri wa Kilimo,
Chakula na Ushirika. Wizara yake inakabiliwa na tuhuma ya kuzembea
kwenye eneo la mashamba ya mpunga katika Kijiji cha Kapunga, Mbarali,
Mbeya.
“Kuna kaburu mwekezaji alinunua shamba hilo lililokuwa la Nafco,
hajalilima matokeo yake analikodisha kwa wanakijiji vipandevipande.
Sasa mtu ataitwaje mwekezaji wakati ni mbangaizaji tu, hii ni kashfa,
wizara ipo na haisemi lolote.
“Naamini ripoti ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji iliyokuwa
ikiongozwa na Profesa Peter Msolwa itaanika madudu yote haya,” kilisema
chanzo.
WANAVYOTAKA WANANCHI Risasi
Jumamosi wiki iliyopita liliingia mitaani kusikiliza maoni ya wananchi
juu ya watu wanaotakiwa kuwa mawaziri kushika nafasi zilizoachwa wazi.
Katika kila wananchi kumi, nane walitaka mawaziri na wizara zao wawe hivi:
Benard Membe, Waziri wa Fedha, Mipango na Uchumi. Asha-Rose Mtengeti
Migiro (Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa), Lazaro
Samuel Nyalandu (Waziri wa Maliasili na Utalii) na Anne Kilango Malecela
(Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi).
Wananchi hao walisema,
Harrison George Mwakyembe na John Pombe Magufuli waendelee kwenye wizara
zao kwa vile utendaji kazi wao ni mzuri, hauna shaka huku wakitaka
George Huruma Mkuchika awe Waziri wa Ulinzi.
“Ila Amos (Gabriel) Makalla awe waziri kamili wa habari, yule mama
(Fenella Mukangala) apelekwe wizara nyingine. Waziri wa Mambo ya Ndani
sisi wananchi tunamwona. Halafu yule mama anaitwa Joanista (Joackim)
Mhagama aingizwe kwenye Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto,”
alisema mkazi wa Kijitonyama, Dar aliyejitambulisha kwa jina la Kadoda,
fundi wa magari, Bamaga, Mwenge.