
Waziri
wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe akionesha picha ya kijana Leonard
Jeremiah Monyo aliyekamatwa na kete 86 za madawa ya kulevya katika
Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.
Stori: Makongoro Oging’ na Haruni Sanchawa
MTANDAO hatari wa unga nchini Tanzania umeshanaswa, kwa sasa
unafanyiwa kazi kwa kasi na Kitengo cha Kudhibiti na Kupambana na Madawa
ya Kulevya, chini ya kamanda wake, Godfrey Nzowa.
Habari njema
kuhusu kunaswa kwa mtandao wa unga, zinakuja baada ya Waziri wa
Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe kufanya kazi nzuri na kuwataja watu
ambao inadaiwa walihusika katika kupitisha madawa ya kulevya Uwanja wa
Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam.
Madawa ya kulevya.
Sekeseke kuu ni kukamatwa kwa Watanzania wawili, Agnes Gerald
‘Masogange’ ambaye ni mwanamitindo na Melisa Edward, nchini Afrika
Kusini, wakiwa na madawa ya kulevya aina ya Crystal Methamphetamine,
yenye uzito wa kg 120, Julai 5, mwaka huu.
Swali kwamba walipitaje JNIA lilijibiwa na Mwakyembe Jumamosi
iliyopita, akafafanua namna Mfumo wa Kamera za Usalama (CCTV),
zilivyonasa ‘uhuni’ uliofanyika, hivyo akawataja watumishi wa Mamlaka ya
Uwanja wa Ndege (TAA), Yusuf Daniel Issa, Jackson Manyonyi, Juliana
Thadei na Mohamed Kalungwana kuhusika, akaagiza wafukuzwe kazi na polisi
kuwakamata.
Baada ya Mwakyembe, moto unaendelea kuwaka na uchunguzi
wa gazeti hili umebaini kuwa mtandao ulionaswa na Kitengo cha Kudhibiti
na Kupambana na Madawa ya Kulevya, unagusa mikoa yote nchini.
Agnes Gerald ‘Masogange’.
Katika mtandao huo, siri kubwa iliyovuja ni majina na jinsi biashara
hiyo haramu inavyoendeshwa mkoa kwa mkoa, wilayani mpaka mitaani,
vilevile wanamichezo na wasanii mbalimbali ambao imeshabainika kwamba
wengi wao wanatumika kusafirisha unga.
Imebainika kwamba mtandao
huo, uligundulika baada ya watu 2,075 kukamatwa katika kipindi cha
Januari hadi Juni mwaka huu (baadhi yao, picha zao zinaonekana ukurasa
wa mbele).
“Watu tuliowakamata kimsingi ni wale wanaotumwa tu. Sasa
wale ndiyo wamewataja mabosi wao, wameeleza siri kubwa,” alisema Kamanda
Nzowa na kuongeza:
Baadhi ya watuhumiwa wa dawa za kulevya.
“Haikuwa kazi rahisi, tulitumia mbinu za kiaskari kuwafanya waeleze
ukweli. Wamesimulia biashara hiyo inavyofanyika, jinsi watu wenye fedha
wanavyowatumia vijana kusafirisha mizigo.
“Tulichobakiza sasa ni
kuwakamata wahusika na kuusambaratisha mtandao wenyewe. Hata sasa
tunachokifanya ni kupambana na huo mtandao wenyewe, mwisho
tutausambaratisha kabisa.”
NI MWAKA WA VITA NZITO
Nzowa, alisema kuwa mwaka huu umeonekana
kuwa na vita nzito kwa sababu kuna lindi kubwa la watu ambao
wamejiingiza katika biashara ya madawa ya kulevya licha ya wengi
kukamatwa na hata baadhi yao kunyongwa katika nchi za China na Pakistan.
Alisema madawa ya kulevya yenye uzito wa kilo 16,824 (tani 16.8)
yamekamatwa kati ya kipindi cha Januari na Juni, mwaka huu, idadi ambayo
ni kubwa kuliko vipindi vyote vilivyopita.
Melisa Edward
Alifafanua kwamba wingi huo usitafsiriwe tu kwamba biashara ya madawa
ya kulevya inatanuka nchini, isipokuwa itazamwe kwa jicho la pili kwa
upana wake jinsi mapambano dhidi ya biashara hiyo yalivyochochewa
makali.
“Udhibiti umekuwa mkubwa sana. Isichukuliwe tu kwamba
biashara inazidi kushika kasi, hapana, haya ni matunda ya kazi ya
udhibiti ambayo inafanyika. Pengine huko nyuma walikuwa wanapishana kwa
wingi zaidi lakini mapambano yalikuwa dhaifu, kwa hiyo wafanyabiashara
hiyo haramu walikuwa wanajitanua tu.
“Ni wajibu wa kila mtu kumwambia mwenzake aachane na hii biashara,
tunapomkamata na ushahidi, hapo anakuwa amekwenda na maji,” alisema
Nzowa.
Akichambua zaidi, Nzowa alisema takwimu za madawa ya kulevya
aina ya heroin zilizokamatwa katika kipindi hicho ni kilo 30 na
washitakiwa ni 45, kati yao wanawake ni wanne.
Alisema, cocaine
walikamata kilo nne na watuhumiwa ni 18 ambao ni wanaume watupu na dawa
aina ya ephedrine walikamata kilo 12 mshitakiwa ni mmoja mwanaume na
bangi ilikamatwa kilo 9,999 na watuhumiwa ni 1,478, kati yao wanawake
ni wawili.
Aliongeza kuwa licha ya kukamata bangi, polisi waliweza
kuharibu ekari 300 za mmea huo katika mikoa ya Arusha, Tanga na Mara
wilayani Tarime.
Baadhi ya watuhumiwa wa madawa ya kulevya
Kamanda Nzowa akaongeza kwamba polisi wanafanya kazi hiyo nzuri kwa kushirikiana na raia wema.
“Hivi sasa tuko makini sana kwa wasanii na wanamichezo wanaotaka
kusafiri kwenda nje ya nchi kwa sababu tumegundua kuwa wanatumika
kutokana na umaarufu wao,” alisema Nzowa.
Akifafanua zaidi, kamanda huyo alisema wana taarifa kwamba hivi sasa
kuna dawa za kulevya za majimaji, hivyo wanaofikiria kusafirisha hizo
kwa njia hiyo wanapaswa kujua kuwa watagundulika.
“Hii ni vita ambayo kila anayelitakia mema taifa hili anapaswa kushiriki kupambana na dawa za kulevya,” alisema Kamanda Nzowa.
KWA NINI VIJANA WENGI WANAKIMBILIA UNGA?
Mtafiti maarufu na
mwelimishaji wa maisha ya vijana na jamii kwa jumla, James Mwang’amba,
alisema kuwa vijana wengi wanaingia katika wimbi la biashara ya madawa
ya kulevya kwa sababu ya kukata tamaa.
“Ukifuatilia maisha ya vijana
kwa sasa, utagundua kwamba wengi wao wamekata tamaa. Wanahisi hawana
njia ya kutoka kimaisha ndiyo maana wanaona fursa yoyote inayokuja mbele
yao inafaa hata kama ni hatari.
“Kila mtu anatamani sana maisha ya juu, awe na kipato kikubwa, sasa
kwa vile haoni njia nzuri za kufikia ndoto zake, anaamua kujiingiza
kwenye usafirishaji wa madawa ya kulevya ili apate fedha za haraka ili
naye awe mtu fulani,” alisema Mwang’amba na kuongeza:
“Tatizo kubwa ni hii tofauti ya kipato. Kuna tofauti kubwa sana kati
ya wenye nacho na wasio nacho, hii ni hatari sana. Sasa jamii kwa vijana
ni hatari zaidi kwa sababu damu inachemka na kuona kila kitu ni rahisi
kufanya.
“Hakuna sababu nyingine kwa nini vijana wengi wanakuwa
wauza unga, ukweli ni tamaa ambayo inachochewa na hasira ya kuwa na
maisha duni wakati wanawaona wengine wakiwa matajiri wakubwa.”