Na Waandishi Wetu VILIO,
majonzi vilitawala katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius
Nyerere (JNIA) Agosti 7, mwaka huu kufuatia kuwasili kwa mwili wa
mwanafunzi wa kidato cha nne, Habiba Yusuph Ally (24) aliyefariki dunia
kwa kubakwa nchini China miezi nane iliyopita.
Mwili wa Habiba Yusuph Ally (24) ukiwa katika jeneza eneo la uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).
Tukio hilo linaweka historia ya kusikitisha kwenye familia ya mzee
Yusuph Ally kwa kuwa na msiba miezi nane wakati mwili wa binti yake
ukiwa mochwari nchini humo baada ya kifo chake.
Habiba Yusuph Ally enzi za uhai wake.
KWA NINI MIEZI NANE? Akizungumza na Uwazi kwa
masikitiko makubwa, baba wa marehemu alisema kilichosababisha maiti ya
binti yake ikae mochwari kwa muda wote huo ni utafutaji wa fedha kuwa
mgumu lakini hatimaye Watanzania waishio nchini humo walifanikisha na
kuuleta kwa ndege ya Shirika la Ndege la Emirates.
Mwili wa Habiba Yusuph Ally ukichukuliwa kutoka uwanja wa ndege.
ALICHOKIONA BABA CHAMSHTUA Mara baada ya mwili
huo kuwasili, kilifika kipengele cha kufunuliwa ili baba mzazi amtambue
marehemu ambapo zoezi hilo lilimshtua mzee huyo kufuatia kuuona uso wa
mwanaye ukiwa na majeraha kibao huku tumbo likiwa limeshonwa. Ilidaiwa
ulifanyiwa uchunguzi.
MWILI WAPELEKWA NYUMBANI Baada ya hapo, mwili
huo ulipekekwa nyumbani kwa mzee Yusuph kwa ajili ya kuagwa na siku
iliyofuata, Agosti 8, mwaka huu ukazikwa kwenye Makaburi ya Magomeni
Mikumi jijini Dar es Salaam.
Mwili wa marehemu, Habiba Yusuph Ally ukipakiwa kwenye gari .
HABIBA ALIVYOKUFA Katika gazeti ndugu na hili,
Ijumaa Wikienda Toleo la Februari 24, mwaka huu liliandika habari ya
kubakwa kwa Habiba hadi kufariki dunia. Habari hiyo ilikuwa na kichwa
cha habari kilichosomeka; MBONGO ABAKWA CHINA, AFA! Kwa mujibu wa baba,
Habiba alibakwa Januari 18, mwaka huu.
Maelezo ya habari hiyo yaliyotolewa na rafiki wa karibu wa Habiba
aitwaye Saada yalisema siku ya tukio, marehemu alikutana na Mnigeria
mmoja ambaye walipatana kulala wote kwa usiku mzima.
Alisema kumbe
Mnaigeria huyo alikuwa na wenzake wanne. Usiku walimwingilia wote kwa
nguvu mpaka akapoteza maisha palepale. Ulikuwa ukatili mkubwa.
Watu hao walipogundua Habiba amefariki dunia waliuchukua mwili wake
na kuutupa chini kutoka ghorofa ya tano walikokuwa wamempeleka kulala
naye.
Baadhi ya waombolezaji wakiwa msibani.
Habari zaidi zilidai kuwa madaktari waliokuwa wakiuchunguza mwili wa
Habiba waligundua haukuwa na figo na moyo jambo lililozidi kuzua hofu
juu ya mauaji yake.
Hata hivyo, kwa mujibu wa mzee Yusuph juzi,
Wanigeria hao walikamatwa na jeshi la polisi nchini humo na kufikishwa
mahakamani kwa kudaiwa kuua.
Alisema mara baada ya kifo, polisi nchini humo waliizua maiti yake
kwa muda ili kupisha upelelezi zaidi na baada ya kukamilika ndipo
Watanzania walioko huko wakaanzisha mchango wa fedha kwa kushirikiana na
Ubalozi wa Tanzania, China na kuusafirisha mwili wake.
MBONGO AONGEA Uwazi lilibahatika kuzungumza kwa
simu na Mtanzania anayeishi kwenye Mji wa Guangzhou nchini China (jina
tunalo) ambaye alidai nguvu kubwa ilitumika kuchangishana fedha ili
kuuleta Bongo mwili wa marehemu Habiba.
Masheikh wakiuswalia mwili wa Habiba kwa safari yake ya mwisho.
ATOA USHAURI Mbongo huyo anayefanya biashara
nchini humo alitoa ushauri kwa Watanzania wenye ndugu China kuwa makini
nao kwa vile wengi wakifa, kama hakuna moyo wa kuchangiana huzikwa na
taasisi zinazosimamia kazi hizo lakini ikibainika kuwa kuna michango
inayoendelea, mwili unaweza kuwekwa mochwari hata miaka miwili.
HISTORIA YA MAREHEMU HABIBA Marehemu Habiba
aliondoka Bongo kwenda China mwaka 2010 akiwa na miaka 19 akisoma kidato
cha nne katika Shule ya Sekondari ya Kiluvya, Kinondoni, Dar kufuatia
kurubuniwa na mwanamke mmoja aliyetajwa kwa jina moja la Chausiku.
Vijana wakiushusha mwili wa Habiba kaburini.
Kwa mujibu wa baba wa marehemu, marehemu Habiba alikuwa mtoto wa tano
kati ya saba, aliondoka nchini na mwanamke huyo bila kumwambia ndugu
yeyote.
“Alirubuniwa na huyo Chausiku kwamba anakwenda kufanya kazi saluni
lakini alipofika kule akamwingiza mwanangu kwenye biashara ya ukahaba.
Hata hao waliombaka walimpata kwenye biashara hiyo,” alisema baba wa
marehemu.
Wakati wa Mazishi ya Habiba.
Akaongeza: “Sisi tukiwa hatujui alipo, miezi minne
ilipita akampigia simu mama yake na kumwambia yupo Dubai anafanya kazi,
tulipochunguza namba ilionesha yupo China, tukaambiwa huwa hawatakiwi
kusema ukweli wa sehemu walipo.”
BIASHARA ILIVYO Uchunguzi unaonesha kuwa,
mawakala wanaosafirisha wasichana wa Kibongo kwenda China, Dubai au
India, wakifika, huwanyang’anya hati zao za kusafiria ili washindwe
kuondoka nchini humo na kushinikizwa kujiuza (ukahaba) huku wao mawakala
wakipokea fedha kutoka kwa wateja.
Uchunguzi unaonesha wasichana hao hurejeshewa hati zao baada ya
malipo ya kiasi cha Dola za Marekani 8,000 (kama shilingi milioni 12).
Marehemu Habiba Yusuph Ally (kushoto) wakati akiwa shule.
Wengi wakishaachiwa hushindwa kurejea Bongo na kujikuta wakiendelea
kuuza miili katika mahoteli na klabu huku wakikutana na majanga
mbalimbali.