Saturday, July 19, 2014

Jaja aanza kazi Yanga, afanya balaa mazoezini

Straika mpya Yanga, Mbrazili, Genilson Santana Santos ‘Jaja’,
Na Sweetbert Lukonge
STRAIKA mpya Yanga, Mbrazili, Genilson Santana Santos ‘Jaja’, tayari ameanza kuonyesha makeke yake baada ya kuonyesha uwezo mkubwa wa kuzifumania nyavu katika mazoezi ya timu hiyo yaliofanyika kwenye Uwanja wa Shule ya Sokondari Loyola, Mabibo, jijini Dar es Salaam, jana.
Jaja, tangu atue hapa nchini Jumanne iliyopita akitokea Brazil, alikuwa hajawahi kufanya mazoezi ya kucheza mpira, siku zote alikuwa akifanya mazoezi ya kukimbia ili kujiweka fiti tayari kwa kuungana na wachezaji wenzake wanaoendelea na programu za kocha wa timu hiyo, Marcio Maximo kwa ajili ya michuano ya ligi kuu msimu ujao na ile ya kimataifa.
Hata hivyo, katika mazoezi ya jana ambayo Jaja alijumuika na wachezaji wenzake katika kuuchezea mpira ikiwa ni mara yake ya kwanza tangu ajiunge na timu hiyo, alionyesha uwezo mkubwa wa kuzifumania nyavu.
Katika mazoezi hayo ambayo wachezaji wa timu hiyo walikuwa wakifundishwa na Maximo jinsi ya kufunga pindi wanapokuwa katika eneo la hatari, Jaja alipiga mashuti nane na matano kati ya hayo yalitinga wavuni.
Mashuti matatu alimfunga Juma Kaseja na mawili alimfunga Ally Mustapha ‘Barthez’, jambo ambalo liliwafanya mashabiki wengi waliokuwa wakiangalia mazoezi hayo kumpigia makofi mchezaji huyo.
Mchezaji mwingine aliyefanya vizuri katika mazoezi hayo alikuwa ni Hamis Thabiti ambaye alizifumania nyavu mara sita na kukosa mashuti miwili.

No comments:

Post a Comment