Monday, January 13, 2014

MAN CITY YAKWEA KILELENI ENGLAND

London, England
NEWCASTLE United jana walishindwa kuuzuia muziki wa Manchester City kwenye Ligi Kuu ya England baada ya kukubali kichapo cha mabao 2-0 kwenye Uwanja wa St James.
Ushindi huu umewafanya City kuongoza ligi hiyo kwa tofauti ya pointi moja dhidi ya Chelsea inayoshika nafasi ya pili baada ya kujikusanyia pointi 47 kati ya 46 za Chelsea.
Hata hivyo, Arsenal ambayo inacheza leo Jumatatu na Aston Villa inaweza kuzishusha timu zote hizo kama itaibuka na ushindi.
Bao la kwanza la City liliwekwa kimiani na mshambuliaji hatari Eden Dzeko, katika dakika ya nane tu ya mchezo baada ya mabeki wa Newcastle kushindwa kuuokoa mpira uliopigwa katikati ya lango lao.
Katika dakika za nyongeza wakati Newcastle wakishambulia kwa nguvu kubwa, Negredo aliambaa na mpira na kuifungia timu yake bao la pili.
Newcastle walionyesha kiwango kizuri kwenye mchezo huo lakini walijikuta wakipoteza nafasi nyingi za wazi.
Hata hivyo, mchezo huo umekuwa pigo kwa City baada ya wachezaji wake wawili, Samir Nasri na Yaya Toure kuumia na kutolewa uwanjani.
Nasri alitolewa kwa machela baada ya kugongwa na Yanga-Mbiwa, huku Toure akitoka mwenyewe baada ya kugongwa na Cheikh Tiote.
Newcastle wapo katika nafasi ya nane wakiwa na pointi 33 baada ya kucheza michezo 21.

No comments:

Post a Comment